Wednesday, June 8, 2011

Uhuru wa vyombo vya habari, bila habari

Na Samson Kamalamo

KILA Mei 3 ya kila mwaka, ulimwengu huwa unaadhimisha Siku ya Uhuru wa vyombo vya habari duniani.

Mwaka huu kaulimbiu ya siku hiyo inasema: “Ukimya unaua demokrasia, lakini vyombo huru vya habari vinazungumza”.

Kimsingi ni kaulimbiu inayojaribu kuchochea vyombo vya habari kuzungumza zaidi na hasa masuala ya kijamii ambayo kwayo yameonekana kusahaulika.

Soma magazeti ya kila siku na kila wiki, sikiliza redio na kama haitoshi angalia matangazo ya vituo mbalimbali vya televisheni; vyote vimesheheni masuala ya siasa, mapigano na mauaji. Hivi ni kweli vyombo vya habari vipo katika kuangazia maeneo hayo tu?

Ni wazi kuna mahala vyombo vya habari vimepoteza mwelekeo na kujikuta vikishindwa kutimiza wajibu wake wa kuwapasha habari wananchi hasa zile zinazowahusu. Sitaki kuamini kuwa wasomaji wa magazeti na wasikilizaji wa redio wanavutiwa zaidi mambo ambayo yamekuwa yakiripotiwa na vyombo hivyo.

Ukweli ni kwamba hawapendi. Sisi wanahabari na mabwana zetu yaani wamiliki, ndiyo tunaoamua kipi tuwalishe wasomaji na wasikilizaji wetu. Hakika hatuwatendei haki hata kidogo.

Kwa upande wa Tanzania Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari uadhimishwa kwa namna nyingi, mojawapo ikiwa ya kuwatunikia Tuzo waandishi walioshinda katika nyanja mbalimbali za uandishi wa habari kwa mwaka mzima.

Hii inawezekana kuwa njia sahihi ya kuenzi siku hii, lakini pia bado kuna mapungufu makubwa katika tasnia hiyo ya habari nchini, kiasi cha Fikra Pevu kusema kuwa ni Siku ya uhuru wa vyombo vya habari, bila habari.

Fikra Pevu inaona ni siku ya uhuru wa vyombo vya habari, bila habari kutokana na ukweli kwamba, ziko habari nyingi ambazo zingepaswa kuandikwa, lakini haziandikwi, na kwamba waandishi wa habari wa Tanzania tunayo fursa ya kuandika mambo mengi ya msingi kuhusu nchi yetu lakini hatuandiki.

Huu ni uzembe unaostahili kupigiwa kelele na kila mwanataaluma na hata hao wanaodhamini mashindano ya wanahabari katika kuadhimisha siku ya uhuru wa vyombo vya habari.

Ingependeza kama kila mwaka kungewekwa agenda za msingi ambazo vyombo vyetu vya habari vingepaswa kuzijadili na kuzizungumzia kwa kina, halafu siku ya uhuru wa vyombo vya habari itumike kama sehemu ya kutathmini mafanikio yaliyofikiwa na hata kushindwa kufanikiwa.

Kwa mfano, ukifuatilia kwa ukaribu vyombo vyote vya habari vya Tanzania kwa miaka takriban mitatu mfululizo, vimekuwa vikiandika na kuripoti kuhusu ufisadi, si kwa kufanya uchunguzi, bali kwa kunukuu wanasiasa wakisema.

Hivi kama kweli ufisadi ni tatizo na watanzania wamechoshwa nao, jitihada gani za makusudi zimefanywa na vyombo vyetu vya habari katika kuhakikisha wanaotuhumiwa kwa ufisadi wanafikishwa katika vyombo vya sheria?

Hapa kuna mchezo wa kupoteza muda na kubadilisha mwelekeo wa fikra za watanzania, kuacha kufikiria mambo ya msingi na kuimbishwa ufisadi kila kukicha.

Kama kweli hatutumiki, basi leo hii mahakama zetu zingekuwa zimesheheni makumi kama si mamia ya kesi za ufisadi. Lakini hilo haliwezekani kwa kuwa vyombo vingine vimekuwa haviandiki habari za kina, zenye ukweli na takwimu za uhakika na za kutosha kushawishi mamlaka husika kuchukua hatua stahiki.

Nadhani ufike wakati sasa, tuachane na kushabikia hoja zinazotolewa na vyama vya siasa zenye lengo la kucheza na akili za watanzania; na vyombo vyetu viandike na kujadili masuala ya msingi.

Kwa kuwa hakuna chama hata kimoja kilichoeleza namna ya kutibu ufisadi, basi agenda za vyombo vya habari nchini zingepaswa kuangazia bei za vyakula, bei za mafuta ya petroli na namna ya kujikwamua na suala zima la mfumuko wa bei. Hayo ndiyo mambo ya msingi kwa watanzania, mambo ambayo hata siku moja hayahubiriwi na vyama tunavyovishabikia.

Siku ya uhuru wa vyombo vya habari kwa Tanzania ingepaswa kuadhimishwa kwa vyombo vya habari kutoa ushuhuda, ni kwa jinsi gani vimeweza kubadili maisha ya watanzania kwa mwaka uliotangualia na vitakavyoendelea kuboresha katika mwaka unaokuja na si kushabikia mitazamo ya kisiasa kama ilivyo sasa.

Wasalaam…

Bajeti itoe unafuu kwa maisha

Na Samson Kamalamo

VIKAO vya Kamati mbalimbali za Bunge vimekuwa vikifanyika katika Ofisi Ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam kwa takriban wiki mbili mfululizo zilizopita.

Kamati hizo, kw akiasi kikubwa zimekuwa zikipitia mapendekezo mbalimbali ya bajeti ya mwaka 2011/20112 pia kupitia ripoti kadhaa za fedha za mashirika ya umma pamoja na halmashauri.

Pasi na shaka, Kamati za Bunge zinazihusika na masuala ya fedha, zimeweza kupitia kwa makini mapendekezo ya bajeti kwa wizara mbalimbali, hivyo jukumu kubwa lililobaki ni kwa Waziri wa Fedha kuwasilisha mapendezo ya jumla bungeni, ili wabunge waanze kujadili.

Ni matumaini ya Fikra Pevu kwamba, bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012 itaangazia zaidi katika kutoa unafuu wa maisha kwa watanzania, ikizingatiwa kuwepo kwa dalili mablimbali za hali ya maisha kuendelea kuwa mbaya hata katika mwaka ujao wa fedha.

Ugumu huo wa maisha unaweza kupimwa kirahisi kwa kuangazi kupanda kwa bei ya mafuta ya petrol kila siku nchini. Ninapoandika waraka huu, tayari katika vile vituo tunavyoweza kusema kwamba vimekuwa vikiwajali zaidi wananchi, bei ya mafuta ya petrol imepanda na kufikia sh 2040/- kwa lita ukiachilia mbali wale wanaouza lita hiyo kwa sh 2070/-.

Kwa wataalamu wa masuala ya uchumi, kupanda kwa bei ya mafuta kwa namna yoyote ile, huwa kunaathiri bei ya bidhaa na huduma nyinginezo muhimu kwa maisha ya binadamu.

Hivyo basi, bei ya mafuta ya petrol inapokuwa juu, ni dhahiri bei ya beidha na huduma mbalimbali nazo huwa zinapanda na kusababisha ugumu wa maisha, kwavile uwezo wa wananchi wa kununua bidhaa kulingana na vipato walivyonavyo pia upungua.

Ni kwa kutambua namna Serikali ya Tanzania ilivyo makini katika kuwajali wananchi wake, tunaamini, kupitia bajeti ya mwaka huu, itakajribu kadri inavyowezekana kuhakikisha kunakuwepo kwa unafuu katika maisha ya watanzania.

Mathalani, kwakuwa moja ya hoja za bei ya mafuta kuwa juu ni kutokana na Serikali kwa kushirikiana na EWURA kuchukua kodi ya takriban sh 600 kwa kila lita, inaweza kupunguza viwango hivyo, na kuwezesha bei ya mafuta kushuka katika soko la ndani.

Lakini pia kwa kuwa bei ya mafuta yanayouzwa nchini huwa inapanda kutokana na muda mwingi unaotumiwa na meli hadi kupakua bandarini, basi kipaumbele cha upakuaji mizigo ungewekwa kwa meli hizo za mafuta, ili zisitumie muda mrefu. Hivyo kupunguza mzigo wanaobebeshwa watanzania na wafanya biashara wa mafuta.

Na zaidi ya hayo, tuamua kuwa mwaka huu wa fedha, ule mpango wa kuagiza mafuta kwa pamoja lazima utekelezwa, ili tuweze kuondokana na sababu za kupanda kwa bei ya mafuta zisizokuwa na msingi.

Naamini, tukisimamia katika eneo hilo la mafuta na kuhakikisha bei yake inashuka, mwaka wa fedha 2011/2012 kwa watanzania utakuwa wa neema, kwavile mfumuko wa bei uaonachangiwa na kupanda kwa bei ya mafuta, utakuwa umedhibitiwa. Zaidi tutabakia kutafuta namna ya kuondokana na vyanzo vingine vya kupandisha mfumuko wa bei.

Fikra Pevu, itaipongeza zaidi serikali endapo bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012 itawawezesha wananchi kuweza kujiweka akiba japo kidogo. Wananchi wakiweza kijiwekea akiba, utakuwa mwanzo wa uchumi kuanza kukua. Wasipoweza kujiwekea akiba, ni wazi kuwa hali yao kiuchumi itakuwa mbaya.

Tunaitakia kila la kheri bajeti ya mwaka 2011/2012 tukiamini kuwa itakuwa ya wananchi zaidi kuliko ya kuwanufaisha wafanyabiashara kama ilivyokuwa ya mwaka 2010/2011.


Serikali iko wapi?

Na Samson Kamalamo

JUMA lililopita, gazeti moja la kila siku, liliripoti kuhusu kukamatwa kwa raia wa Marekani, huko Tarime katika eneo la Nyamongo au North Mara.

Gazeti hilo liliendelea kubainisha kuwa Mmarekani huyo alikamatwa akipiga picha za matukio ya mgodi huo na kuzituma kwenda nchini kwao, haijulikani kwa matumizi gani.

Haikuelezwa kama Mmarekani huyo alikuwana kibali kutoka Idara ya Habari (MAELEZO) kumwezesha kupiga picha katika maeneo mbalimbali ya nchi tena akiwa pekee yake na kuzituma popote anapopenda.

Ninachofahamu, ni kwamba, wote wanaokuja nchi hii wakiwa waandishi wa habari au watu wengine lakini wakiwa na dhamira ya kupiga picha, wanapaswa kuwa na vibali maalum vya maeneo husika, na mara nyingi huambatana na maofisa husika, ili kuhakikisha picha zinazopigwa ni zile tu zilizoombewa kibali.

Katika hili, FIKRA PEVU haina budi kuuliza, Serikali iko wapi? Serikali inayozungumziwa hap si lazima iwe ile kuu, isipokuwa hata zile za vijiji. Ziko wapi, kiasi cha kuruhusu mgeni kufanya anachotaka katika ardhi ya nchi huru kama Tanzania?

Kitendo cha Mmarekani yule kukamatwa akifanya shughuli zake hizo hata kama ni kwa kofia ya kikundi au chama fulani, ni cha kihaini na hakipaswi kuvumbiwa macho na kuachiwa kimalizike hivi hivi tu.

Huu sasa ndiyo wakati wa kuonyesha hao wenye vikundi na washirika wawageni hao kwamba Serikali iko makini na kwamba itasimamia katika sheria na kanuni zilizopo.

Hakuna njia mbadala ya kuonyesha makucha hayo ya serikali isipokuwa kwa Mmarekani huyo na washirika wake wazalendo, wote kwa pamoja kufunguliwa mashitaka ya uhaini na kufikishwa mahakamani mapema iwezekanavyo.

Sidhani kama iko haja ya kuchelewesha jambo hilo, eti kwa visingizio vya kusubiri kukamilika kwa upepelezi. Ni upelelezi gani utatakiwa kufanyika ilhali mtuhumiwa kakutwa na ngozi?

Ngozi yake ni kamera na vifaa vingine vya mawasiliano alivyokutwa navyo eneo la tukio, vinavyomwezesha kuwasiliana na mahali popote pale ulimwenguni.

Mmarekani huyo na wengine wote walioshirikiana naye kwa misingi kwamba wanaweza kufanya lolote bila kufanywa chochote, lazima achukuliwe hatua za kisheria, hili iwe fundisho kwa wengine wanaodhani serikali imelala.

Tujiulize, ni wageni wangapi wamekuwa wakitumiwa na vikundi hivi kuchafua taswira ya Tanzania katika anga za kimataifa? Bila shaka wapo wengi, lakini kwa huyu, arobani yake imefika.

Kukakatwa kwa huyo Mmareni kunapaswa kutumiwa kama taarifa muhimu katika kubaini kwamba nchi yetu imekuwa ikiingiliwa na kuchafuliwa na watu wengi pasipo watanzania wenyewe kujua.

Hii ni dhahiri kwamba vikundi, mashirika yasiyo ya kiserikali, makampuni na hata vyama vya siasa, ama kwa kujua au kutokujua, vimekuwa vikiwezesha Tanzania kuzungumzwa vibaya huko nje na kuonekana kuwa ni taifa lisilostahili kuwepo.

Kuendelea kuvumilia vitendo vya namna hii pasipo kuvichukulia hatua kali ni sawa na kuwasaliti watanzania. Tufike mahali basi, siasa ikae pembeni na sheria ichukue mkondo wake.

Tukiendelea kuikumbatia siasa na kudhani kuruhusu kuwepo kwa maandamano kila kukicha kuwa ndiyo kuimarisha na kukuza demokrasi, huk ni kujidanganya. Ukweli tunajichimbia kaburi letu wenyewe.

Tufike mahali tupime. Na tufike mahali kubainishe wazi upi wakati wa siasa za nje yaani za majukwani na upi wakati wa siasa za ndani. Mbona huko demokrasia ilikopea hatuoni haya yanayotokea kwetu?

Fikra Pevu inaisii serikali iliyoko madarakani kuongeza uamkini kidogo na kusimamia katika sheria, hata kama kwa kufanya hivyo itaonekana kuwa inaminya demokrasia. Hiki kinachotokea sidhani kama ni demokrasia. Ni demokrasia ya wapi inayoruhusu mtu kugusa pua ya mwenzie?

Tuonane wiki ijayo. Wasalaa.

yl� o t H3 ��� 0pt;font-family:"Times New Roman","serif"'>

Hii ni dhahiri kwamba vikundi, mashirika yasiyo ya kiserikali, makampuni na hata vyama vya siasa, ama kwa kujua au kutokujua, vimekuwa vikiwezesha Tanzania kuzungumzwa vibaya huko nje na kuonekana kuwa ni taifa lisilostahili kuwepo.

Kuendelea kuvumilia vitendo vya namna hii pasipo kuvichukulia hatua kali ni sawa na kuwasaliti watanzania. Tufike mahali basi, siasa ikae pembeni na sheria ichukue mkondo wake.

Tukiendelea kuikumbatia siasa na kudhani kuruhusu kuwepo kwa maandamano kila kukicha kuwa ndiyo kuimarisha na kukuza demokrasi, huk ni kujidanganya. Ukweli tunajichimbia kaburi letu wenyewe.

Tufike mahali tupime. Na tufike mahali kubainishe wazi upi wakati wa siasa za nje yaani za majukwani na upi wakati wa siasa za ndani. Mbona huko demokrasia ilikopea hatuoni haya yanayotokea kwetu?

Fikra Pevu inaisii serikali iliyoko madarakani kuongeza uamkini kidogo na kusimamia katika sheria, hata kama kwa kufanya hivyo itaonekana kuwa inaminya demokrasia. Hiki kinachotokea sidhani kama ni demokrasia. Ni demokrasia ya wapi inayoruhusu mtu kugusa pua ya mwenzie?

Sunday, October 24, 2010

Fainali imewadia, uamuzi wakwako

KWA takriban miezi mitatu, magazeti na vyombo vingine vya habari nchini, vimekuwa vikinadi siasa za vyama mbalimbali katika matoleo na machapisho yao.

Hicho kilikuwa kipindi cha kampeni kwa wagombea wa nafasi za urais, ubunge na udiwani, kila mmoja akijaribu kujiuza ili apate kununuliwa. Ndiyo biashara matangazo, na wagombea walikuwa na kila sababu ya kujitangaza ili kwanza wafahamike, lakini pili wakubalike na tatu wanunulike au wachagulike.

Mbinu za kila aina tumeshuhudia zikitumika katika kujinadi huko, zikiwemo safi na chafu, ili mradi mgombea atengeneze mazingira ya kuwa na mvuto kwa wapiga kura.

Wapo baadhi ya wagombea, tunawajua, walidiriki hata kudandia mambo ya uongo yaliyozushwa katika jamii, kwa lengo la kuyatumi akama silaha ya maangamizi dhidi ya viogozi wengine, lakini katika kipindi kifupi tu waliweza kuumbuka, baada ya ukweli wa mambo kuwekwa wazi.

Najua na ninatambua kuwa siku zote kama ilivyo katika vilabu vya mpira wa miguu, huwa wapo washabiki damu. Washabiki ambao huwa hawasiki la mwazini wala la mnadi sala. Wako tayari kushabikia jambo fulani hata kama halina ukweli na maslahi kwa nchi. Hawa hatuna jinsi ya kuwabadili msimamo wao na si makusudi ya safu hii kuwabadili watu hao.

Ninachotaka kusema ni kuwa, tumebakiza siku tano tu kufanya maamuzi makubwa na mazito kwa nchi yetu. Naamini kila mmoja wetu kwa njia moja ama nyingine ameshiriki katika kampeni zilizoanza Augosti 20 mwaka huu hata kama si moja kwa moja au kwa kuhudhuria mikutano ya kampeni katika viwanja mbalimbali.

Ni wazi kuwa hapo ulipo sasa tayari umekwisha kufahamu mgombea yupi unapaswa au ungependa kumchagua ili awe kiongozi wako kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Uamuzi ni wako na una kila sababu ya kuwa huru, lakini unapaswa kujiuliza mara mbili, je huyo unayetaka kumchagua ni kwa kiasi gani ataweza kutimiza ahadi alizotoa majukwaani?

Ni vema ukajiuliza katika hili, ili usije ukafanya maamuzia mbayo pengine yataturudisha nyuma kuliko hapa tulipofikia. Ukidhani kwamba mgombea kipenzi chako anaweza kuleta mabadiliko katika Kata yako, Jimbo na hata nchi basi jitokeze kupiga kura ifikapo Oktoba 31, mwaka huu.

Hapa nina maana kwamba, pamoja na uamuzi ulijikita katika kichwa chako hivi sasa, bado unayo fursa ya kutumia hizi siku tano zilizobakia kumpima mgombea udiwani, ubunge na urais ambaye ndiye chaguo lako kama anafaa. Wakati mwingine si lazima kumchagua swahiba wako kuwa kiongozi endapo uanamini au unadhani kuwa hawezi kutimiza ndoto zako.

Tunachopaswa kufahamu ni kuwa, ushabiki wa aina yoyote ile haupaswi kutawala mawazo, fikra na maamuzi yetu katika kuchagua viongozi. Nafikiri tunapaswa kuwa makini zaidi katika kipindi hiki kuliko wakati mwingine wowote, kwakuwa kosa tutakalolifanya litatugharimu kwa miaka mitano ijayo, labda tu itokeo vinginevyo.

Shime mtanzania mwenzangu usiweke nyuma na kushindwa kupiga kura Oktoba 31. Endapo utakuwa mzima wa afya, jitokeze wewe na familia yako na wote waliofikisha umri wa kupiga kura, kutumia haki yenu hiyo ya msingi, kikatiba na kidemokrasi ya kuingiza viongozi madarakani, kwa umakini mkubwa.

Nasisitiza upige kura kwa umakini kwakuwa ukishapiga kura na kwa bahati mbaya ukafanya uchaguzi batili, hautakuwa na fursa ya kufanya mabadiliko kwakuwa mfumo huo wa demokrasia haupo na haujapata kutumika katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Itakulazimu kusubiri kwa miaka mitano ndipo ujisahihishe.

Waungwana, fainali imewadia, uamuzi ni wa kwako. Jitahidi kufanya maamuzi sahihi, ili uendelee kuwa na furaha katika miaka mitano ijayo. Furaha na majuto yako mikononi mwako, huna sababu ya kujuta wakati fimbo unayo mkononi. Kila la kheri katika uchaguzi mkuu, usibaki nyumbani, jitokeze kupiga kura kumchagua yule unayeona anafaa kuwa kiongozi wa eneo lako, jimbo na hata nchi.

Wasalaam,

Tunahitaji serikali ndogo, makini

HAPANA shaka singo mpya za kampeni ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, zinaelekea ukingoni kusikika. Kwa ambao hawakupata bahati ya kurusha singo zao, wasubiri 2015.

Kumalizika kwa singo hizo, hakuashirii kitu kingine chochote, zaidi ya kupata serikali mpya, wabunge na madiwani wapya.

Kupatikana na kwa serikali mpya, yaani Rais aliyeko madarakani kuchaguliwa tena kwa kipindi cha miaka mitano au kuchaguliwa kwa Rais mpya kabisa, jambo ambalo si rahisi kutokea kwa mazingira yetu kwa sasa, kunaibua hisia na matumaini mapya ya wananchi juu ya serikali hiyo.

Ni kwa kutambua kwamba watanzania watakuwa na hisia na matumaini mapya kutoka kwa yoyote atakayeshikilia usukani huo wa urais, nimeona iko haja ya kutumia safu hii kueleza nini watanzania tunahitaji kutoka kwa Rais huyo.

Ama kwa mtazamo wa safu hii kama nilivyoeleza hapo awali, hapana shaka hata kidogo, Rais aliyeko madarakani, Jakaya Kikwete atarejea tu hata kwa ushindi mwembamba wa kura mbili dhidi ya wapinzania wake.

Ukweli hili halina ubishi, kwamba tukiangazia matokeo kura za maoni yaliyoendeshwa na mashirika mbalimbali ya utafiti nchini yakiwemo REDET na Synovate.

Kwa matokeo yale, licha ya kuwepo kwa kauli za hapa na pale za wanaojiita wanaharakati wa kutetea haki na maslahi ya watanzania, bado hakuna ubishi kati ya wagombea wanaoshindana na JK hakuna wa kumshinda.

Inaweza kusemwa kwamba nimekurupuka kuweka bayana kile ninachoamini, lakini kwa mazingira ya Tanzania na Afrika kwa ujumla, hata Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), itakubaliana nami kuwa upinzani bado hauna nafasi.

Ndiyo, historia inaonyesha kuwa upinzani ulipata kufanikiwa Kenya, Zambia na Malawi tukizungumzia mifano michache, lakini huko kwa wenzetu kuna mazingira tofauti. Kwa waliofika katika nchi hizo wanatambua na hata wapinzani wenyewe wanatambua.

Kwa Tanzania kuwa na madiliko ya Chama itatuchukua muda mrefu kutokana na sababu nyingi, mojawapo ikiwa ni ya uelewa finyu au duni wa sera na mchakato mzima wa mfumo wa siasa ya vyama vingi. Vyama vyetu kama vilivyo vyombo vyetu vya habari, bado ni vya wakazi wa mijini tu. Huu ndiyo ukweli, na kwa jinsi hii, upinzani utafanikiwa pale utakapoweza kuwafikia asilimia 50 ya watanzania.

Kwa kuwa hakuna takwimu sahihi za idadi gani ya watanzania wamefikiwa na kuelimishwa kuhusu mfumo wa siasa wa vyama vingi na umuhimu wake kwao na maendeleo yao, bado tutalazimika kukubali kuendelea kuongozwa na CCM, na kwa maana hiyo, hatuna sababu ya kukwepa adui kama anavyofanya Mbuni kwa kufukia kichwa huku kiwiliwili kiko hadharani.

Kwa vile dalili zipo kuwa JK atatuongoza kwa miaka mingine mitano na kwa kuwa yapo mengi yamesemwa mtaani kuhusu awamu ya kwanza ya serikali ya Kikwete, iko haja ya kuwepo kwa mabadiliko katika awamu ya pili ya uongozi wake.

Katika awamu hiyo, safu hii, ingemshauri JK aunde Baraza dogo la Mawaziri, makini ambalo litakuwa tayari kutekeleza maagizo atakayokuwa anatoa. Baraza hilo kuundwa na timu kubwa ya watu kutokana wabunge kumi ambao Kikatiba, JK atakuwa na haki ya kuwateua.

Safu hii inapendeza hivyo kwa kuamini kuwa, wabunge utakao wateua kutoka miongoni kwa watanzania milioni 40 wenye sifa ya kuwa viongozi, lakini kwa sababu mbalimbali wameshindwa kuingia kwenye siasa, hapa shaka watakuwa mawaziri na watendaji wazuri na hawatakuwa tayari kukuangusha kwa lolote, kwa kuwa hawatakuwa na jeuri ya kusema kuwa wamechaguliwa na wananchi.

Hata hivyo, unaweza kuteua wabunge kutoka katika majimbo kuwa mawaziri, lakini kigezo kikubwa kikiwa uadilifu wao kwako na kwa watanzania, utendaji na utayari wao wa kulitumia taifa hili kwa moyo mmoja, kama ilivyopata kuwa kwa John Magufuli wakati ule akiwa Waziri wa Ujenzi.

Hizo ndizo salamu za safu hii kwako na kukukumbusha kuwa kweli rafiki ni bora lakini si mara zote. Wakati mwingine anaweza kuwa kikwazo cha wewe kufikia mafanikio au malengo uliojiwekea.

Nawatakia maandalizi mema ya kupiga kura Oktoba 31, mwaka huu.

NEC teknolojia izae matunda mema

JUMA lililopita Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilitangaza kwamba matokeo ya kura za urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu yatakuwa ya kwanza kutolewa kabla ya matokeo ya ubunge na udiwani.

Kwetu watanzania hii ni faraja kubwa ikizingatiwa kwamba katika miaka iliyopita, matokeo yalichukua siku tano hadi kumi kutokana na mfumo wa ukusanyaji taarifa za matokeo ulivyokuwa, pamoja na jiografia ya nchi yetu.

Mwaka huu NEC imeamua kutumia teknolojia ya kisasa ya mawasiliano ambapo haichukui muda mrefu kwa matokeo ya kura za aina yoyote kuweza kuwekwa bayana kwa taasisi na jamii husika.

Haya naweza kusema ni mapinduzi, kwakuwa yatatuwezesha watanzania kumfahamu kiongozi mpya wa Tanzania katika kipindi kifupi baada ya watanzania kutumia haki yao ya msingi ya kumchagua Rais wao.

Ni dhahiri kuwa wapiga kura 19,686,608 waliojiandikisha kwa ajili ya kupiga kura Oktoba 31 mwaka huu, watakuwa na fursa nzuri ya kutambua matokeo ya maamuzi yao, pasipo kuwepo kwa uwezekano wa namna yoyote ile ya matokeo hayo kuchakachuliwa.

Fikra Pevu inaipongeza NEC kwa utaratibu huo mpya, kwakuwa umekuja wakati muafaka na inaamini kuwa utaondoa fikra za kuwepo kwa mazingira ya kura za rais kuchezewa na kutolewa matokeo yasiyo haki.

Ni kwa mantiki hii, vyama vya siasa nchini vinapaswa kujiweka tayari kupokea matokeo yoyote yatakayotolewa na NEC, siku moja baada ya watanzania kupiga kura.

Hatutarajii kwa vyovyote vile baada ya matokeo hayo ya urais kutangazwa tena kwa kushirikisha mawakala wa vyama katika vituo vyote vya kupigia kura, kutajitokeza madai ya kutokukubalina na matokeo yatakayotangazwa.

Ni vema kupitia uchaguzi huu wa nne wa demokrasia ya vyama vingi, wanasiasa na hasa wagombea, wakajifunza namna ya kukubali matokeo hata kama yatakuwa kinyume cha matarajio yao.

Kukubali matokeo, ni dalili za kukomaa kisiasa na hakuna sababu kwa wanasiasa wa Tanzania kuendelea kuwa wachanga ilhali mfumo wa siasa za Tanzania unaendelea kukua na kuimarika kila siku.

Kwakuwa NEC imeamua kutumia mfumo mpya wa kuwezesha kupatikana kwa matokeo kwa muda mfupi zaidi, ni wazi kuwa mfumo huo utazaa matunda mema na utakuwa chachu ya mabadiliko na maendeleo ya kidemokrasia nchini Tanzania.

Kama ambavyo teknolojia ya mawasiliano ilivyoweza kufanya kazi vema nchini Kenya mwaka 2007, ndivyo ambavyo tunaamini itatumika kutoa matokeo mema katika uchaguzi mkuu wa Tanzania mwaka huu.

Kwa utaratibu huu, tunaamini watanzania watakuwa na fursa ya kukwenda sanjari na mabadiliko ya kiteknolojia ambayo siku zote yanaaminika kutoa matokeo sahihi endapo hapatakuwepo na wajanja wachache watakaoamua kucheza matokeo hayo kwa maslahi yao binafsi.

Fikra Pevu inaamini kuwa hapatakuwepo na uchezeaji wa namna yoyote wa matokeo ya uchaguzi wa mwaka huu, ili kupunguza uwezekano wa kuwepo au kujitokeza kwa malalamiko ya aina yoyote ile. Kama upo uwezekano wa kuepuka malalamiko, basi nguvu za ziada zitumike kuondosha malalamiko ya aina hiyo.

Rai ya safu hii ni kwamba NEC itumie hiyo teknolojia mpya katika kuharakisha kupatikana kwa matokeo, izae matunda mema na si machungu.

Tuonane Juma lijalo.

Ahadi sawa, mbichi au mbivu juu yetu

NINAPOANDIKA waraka huu, zimebaki siku 25 tu kwa watanzania kutafakari hatima ya taifa lao.

Zitakapokwisha siku hizo 25, ile ya 26 yaani Oktoba 31, itakuwa ni siku ya kufanya maamuzi mazito juu ya taifa hili linaloendelea.

Ni siku ya kila mtanzania aliyejiandikisha kupiga kura na ambaye jina lake lipo sahihi katika daftari la wapiga kura, atatumia haki yake ya kikatiba ya kumchagua yule anayedhani anafaa kuwa kiongozi wa taifa ili kwa miaka mitano ijayo.

Tunapozungumzia uchaguzi, mara nyingi tunazungumzia Rais,Wabunge na Madiwani. Lakini katika muktadha huu wa leo, nataka tu kuwakumbusha watanzania kuwa makini katika kufanya maamuzi hayo mazito.

Kimsingi ni maamuzi ambayo hayahitaji kufanyiwa majaribio, ukitaka kufanya majaribio, majuto yatakuwa haki yako, na usipojitokeza kabisa kupiga kura, hautakuwa na haki ya kuinua mdomo kulaumu maamuzi watakayokuwa wamefikia wenzako.

Pamoja na kwamba uchaguzi unahusu wagombea urais, ubunge na udiwani, mkazo mkubwa upo katika kuchagua nani awe Rais wa nchi katika kipindi cha uongozi wa miaka mitano kuanzia mwaka 2010.

Najua na ninatambua kuwa kuanzia Agosti 20 mwaka huu tumekuwa tukisikia na kuwaona wanasiasa wengi wakisimama majukwaani kunadi sera na ilani za vyama vyao. Hawakuishia hapo, wengi wao wamekwenda mbali kiasi cha kutoa ahadi kemkem.

Kweli ahadi ni sawa kabisa. Hata sisi wenyewe kwa wenyewe mara nyingine tumekuwa tupeana ahadi mbalimbali za kutiana moyo, lakini tujiulize ni mara ngapi ahadi hizo zimepata kutimizwa.

Kwa kuwa wengi wetu tupo masikini, na hatuna uwezo, tumejikuta ahadi zetu nyingi zikiyeyukia hewani kwa kukosa nyezo za kutumia katika kuzitekeleza. Zimebaki kuwa ahadi hewa.

Ni kwa kigezo hicho, ndipo napotaka kuwaasa watanzania wenzangu kuwa makini katika kutumia hiyo haki yao ya kikatiba.

Ni vema mkatumia muda huu uliobaki wa siku 25 kupima ahadi zilizotolewa na wagombea mbalimbali wa nafasi ya Urais, kupata uhakika wake wa kuweza kutimizika.

Nisingependa mzipime ahadi hizo kwa uzuri wake wa mapambo ya lugha zilizotumika, bali kwa uhalisia wake kwa kuzingatia mazingira ya Tanzania na uwezekano wa kutekelezeka kwake.

Tuwapime wagombea wetu kwa kutumia vigezo mbalimbali, ambapo yule tutakayeona anayo nafasi kubwa ya kutimiza ahadi zake, basi tumpe fursa hiyo, badala ya kuwapa wengine ambapo kwa hakika itawalazimu watumie muda mwingi kujipanga hadi waje kufikia hatua ya kuanza kutekeleza ahadi zao hizo.

Ikumbukwe kuwa katika ulimwengu wa siasa, hakuna muda wa majaribio. Muda uliopo kila siku ni wa kutenda na kutekeleza ahadi zilizopo na zinazotolewa.

Hofu yangu ni kwamba, tusije tukatumia njia ndefu kupata maji ya kukata kiu yetu, wakati maji tayari tunayo mkono. Tunachotakiwa ni kujadiliana jinsi ya kuendelea kuyanywa tena tukiwa tumejikalia kivulini.

Hivyo basi, ni juu yetu watanzania kuchagua mbichi au mbivu ifikapo tarehe 31 Oktoba, 2010. Uamuzi unao mwenyewe, usipojitokeza utakuwa ujinga wako na ukimchagua atakayekuja kukurudisha nyuma ni uzembe, kwa kuwa utakuwa umepoteza muda, ambao ni kutu cha thamani sana kuliko kingine katika maisha yako.

Siku ya siku ikifika, tujitokeze kwa wingi na tufanye maamuzi sahihi pasipo kushawishiwa au kurubuniwa wa yeyote. Zimwi likujualo halikuli likakwisha.