HAPANA shaka singo mpya za kampeni ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, zinaelekea ukingoni kusikika. Kwa ambao hawakupata bahati ya kurusha singo zao, wasubiri 2015.
Kumalizika kwa singo hizo, hakuashirii kitu kingine chochote, zaidi ya kupata serikali mpya, wabunge na madiwani wapya.
Kupatikana na kwa serikali mpya, yaani Rais aliyeko madarakani kuchaguliwa tena kwa kipindi cha miaka mitano au kuchaguliwa kwa Rais mpya kabisa, jambo ambalo si rahisi kutokea kwa mazingira yetu kwa sasa, kunaibua hisia na matumaini mapya ya wananchi juu ya serikali hiyo.
Ni kwa kutambua kwamba watanzania watakuwa na hisia na matumaini mapya kutoka kwa yoyote atakayeshikilia usukani huo wa urais, nimeona iko haja ya kutumia safu hii kueleza nini watanzania tunahitaji kutoka kwa Rais huyo.
Ama kwa mtazamo wa safu hii kama nilivyoeleza hapo awali, hapana shaka hata kidogo, Rais aliyeko madarakani, Jakaya Kikwete atarejea tu hata kwa ushindi mwembamba wa kura mbili dhidi ya wapinzania wake.
Ukweli hili halina ubishi, kwamba tukiangazia matokeo kura za maoni yaliyoendeshwa na mashirika mbalimbali ya utafiti nchini yakiwemo REDET na Synovate.
Kwa matokeo yale, licha ya kuwepo kwa kauli za hapa na pale za wanaojiita wanaharakati wa kutetea haki na maslahi ya watanzania, bado hakuna ubishi kati ya wagombea wanaoshindana na JK hakuna wa kumshinda.
Inaweza kusemwa kwamba nimekurupuka kuweka bayana kile ninachoamini, lakini kwa mazingira ya Tanzania na Afrika kwa ujumla, hata Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), itakubaliana nami kuwa upinzani bado hauna nafasi.
Ndiyo, historia inaonyesha kuwa upinzani ulipata kufanikiwa Kenya, Zambia na Malawi tukizungumzia mifano michache, lakini huko kwa wenzetu kuna mazingira tofauti. Kwa waliofika katika nchi hizo wanatambua na hata wapinzani wenyewe wanatambua.
Kwa Tanzania kuwa na madiliko ya Chama itatuchukua muda mrefu kutokana na sababu nyingi, mojawapo ikiwa ni ya uelewa finyu au duni wa sera na mchakato mzima wa mfumo wa siasa ya vyama vingi. Vyama vyetu kama vilivyo vyombo vyetu vya habari, bado ni vya wakazi wa mijini tu. Huu ndiyo ukweli, na kwa jinsi hii, upinzani utafanikiwa pale utakapoweza kuwafikia asilimia 50 ya watanzania.
Kwa kuwa hakuna takwimu sahihi za idadi gani ya watanzania wamefikiwa na kuelimishwa kuhusu mfumo wa siasa wa vyama vingi na umuhimu wake kwao na maendeleo yao, bado tutalazimika kukubali kuendelea kuongozwa na CCM, na kwa maana hiyo, hatuna sababu ya kukwepa adui kama anavyofanya Mbuni kwa kufukia kichwa huku kiwiliwili kiko hadharani.
Kwa vile dalili zipo kuwa JK atatuongoza kwa miaka mingine mitano na kwa kuwa yapo mengi yamesemwa mtaani kuhusu awamu ya kwanza ya serikali ya Kikwete, iko haja ya kuwepo kwa mabadiliko katika awamu ya pili ya uongozi wake.
Katika awamu hiyo, safu hii, ingemshauri JK aunde Baraza dogo la Mawaziri, makini ambalo litakuwa tayari kutekeleza maagizo atakayokuwa anatoa. Baraza hilo kuundwa na timu kubwa ya watu kutokana wabunge kumi ambao Kikatiba, JK atakuwa na haki ya kuwateua.
Safu hii inapendeza hivyo kwa kuamini kuwa, wabunge utakao wateua kutoka miongoni kwa watanzania milioni 40 wenye sifa ya kuwa viongozi, lakini kwa sababu mbalimbali wameshindwa kuingia kwenye siasa, hapa shaka watakuwa mawaziri na watendaji wazuri na hawatakuwa tayari kukuangusha kwa lolote, kwa kuwa hawatakuwa na jeuri ya kusema kuwa wamechaguliwa na wananchi.
Hata hivyo, unaweza kuteua wabunge kutoka katika majimbo kuwa mawaziri, lakini kigezo kikubwa kikiwa uadilifu wao kwako na kwa watanzania, utendaji na utayari wao wa kulitumia taifa hili kwa moyo mmoja, kama ilivyopata kuwa kwa John Magufuli wakati ule akiwa Waziri wa Ujenzi.
Hizo ndizo salamu za safu hii kwako na kukukumbusha kuwa kweli rafiki ni bora lakini si mara zote. Wakati mwingine anaweza kuwa kikwazo cha wewe kufikia mafanikio au malengo uliojiwekea.
Nawatakia maandalizi mema ya kupiga kura Oktoba 31, mwaka huu.
No comments:
Post a Comment