NINAPOANDIKA waraka huu, zimebaki siku 25 tu kwa watanzania kutafakari hatima ya taifa lao.
Zitakapokwisha siku hizo 25, ile ya 26 yaani Oktoba 31, itakuwa ni siku ya kufanya maamuzi mazito juu ya taifa hili linaloendelea.
Ni siku ya kila mtanzania aliyejiandikisha kupiga kura na ambaye jina lake lipo sahihi katika daftari la wapiga kura, atatumia haki yake ya kikatiba ya kumchagua yule anayedhani anafaa kuwa kiongozi wa taifa ili kwa miaka mitano ijayo.
Tunapozungumzia uchaguzi, mara nyingi tunazungumzia Rais,Wabunge na Madiwani. Lakini katika muktadha huu wa leo, nataka tu kuwakumbusha watanzania kuwa makini katika kufanya maamuzi hayo mazito.
Kimsingi ni maamuzi ambayo hayahitaji kufanyiwa majaribio, ukitaka kufanya majaribio, majuto yatakuwa haki yako, na usipojitokeza kabisa kupiga kura, hautakuwa na haki ya kuinua mdomo kulaumu maamuzi watakayokuwa wamefikia wenzako.
Pamoja na kwamba uchaguzi unahusu wagombea urais, ubunge na udiwani, mkazo mkubwa upo katika kuchagua nani awe Rais wa nchi katika kipindi cha uongozi wa miaka mitano kuanzia mwaka 2010.
Najua na ninatambua kuwa kuanzia Agosti 20 mwaka huu tumekuwa tukisikia na kuwaona wanasiasa wengi wakisimama majukwaani kunadi sera na ilani za vyama vyao. Hawakuishia hapo, wengi wao wamekwenda mbali kiasi cha kutoa ahadi kemkem.
Kweli ahadi ni sawa kabisa. Hata sisi wenyewe kwa wenyewe mara nyingine tumekuwa tupeana ahadi mbalimbali za kutiana moyo, lakini tujiulize ni mara ngapi ahadi hizo zimepata kutimizwa.
Kwa kuwa wengi wetu tupo masikini, na hatuna uwezo, tumejikuta ahadi zetu nyingi zikiyeyukia hewani kwa kukosa nyezo za kutumia katika kuzitekeleza. Zimebaki kuwa ahadi hewa.
Ni kwa kigezo hicho, ndipo napotaka kuwaasa watanzania wenzangu kuwa makini katika kutumia hiyo haki yao ya kikatiba.
Ni vema mkatumia muda huu uliobaki wa siku 25 kupima ahadi zilizotolewa na wagombea mbalimbali wa nafasi ya Urais, kupata uhakika wake wa kuweza kutimizika.
Nisingependa mzipime ahadi hizo kwa uzuri wake wa mapambo ya lugha zilizotumika, bali kwa uhalisia wake kwa kuzingatia mazingira ya Tanzania na uwezekano wa kutekelezeka kwake.
Tuwapime wagombea wetu kwa kutumia vigezo mbalimbali, ambapo yule tutakayeona anayo nafasi kubwa ya kutimiza ahadi zake, basi tumpe fursa hiyo, badala ya kuwapa wengine ambapo kwa hakika itawalazimu watumie muda mwingi kujipanga hadi waje kufikia hatua ya kuanza kutekeleza ahadi zao hizo.
Ikumbukwe kuwa katika ulimwengu wa siasa, hakuna muda wa majaribio. Muda uliopo kila siku ni wa kutenda na kutekeleza ahadi zilizopo na zinazotolewa.
Hofu yangu ni kwamba, tusije tukatumia njia ndefu kupata maji ya kukata kiu yetu, wakati maji tayari tunayo mkono. Tunachotakiwa ni kujadiliana jinsi ya kuendelea kuyanywa tena tukiwa tumejikalia kivulini.
Hivyo basi, ni juu yetu watanzania kuchagua mbichi au mbivu ifikapo tarehe 31 Oktoba, 2010. Uamuzi unao mwenyewe, usipojitokeza utakuwa ujinga wako na ukimchagua atakayekuja kukurudisha nyuma ni uzembe, kwa kuwa utakuwa umepoteza muda, ambao ni kutu cha thamani sana kuliko kingine katika maisha yako.
Siku ya siku ikifika, tujitokeze kwa wingi na tufanye maamuzi sahihi pasipo kushawishiwa au kurubuniwa wa yeyote. Zimwi likujualo halikuli likakwisha.
No comments:
Post a Comment