Sunday, October 24, 2010

Fainali imewadia, uamuzi wakwako

KWA takriban miezi mitatu, magazeti na vyombo vingine vya habari nchini, vimekuwa vikinadi siasa za vyama mbalimbali katika matoleo na machapisho yao.

Hicho kilikuwa kipindi cha kampeni kwa wagombea wa nafasi za urais, ubunge na udiwani, kila mmoja akijaribu kujiuza ili apate kununuliwa. Ndiyo biashara matangazo, na wagombea walikuwa na kila sababu ya kujitangaza ili kwanza wafahamike, lakini pili wakubalike na tatu wanunulike au wachagulike.

Mbinu za kila aina tumeshuhudia zikitumika katika kujinadi huko, zikiwemo safi na chafu, ili mradi mgombea atengeneze mazingira ya kuwa na mvuto kwa wapiga kura.

Wapo baadhi ya wagombea, tunawajua, walidiriki hata kudandia mambo ya uongo yaliyozushwa katika jamii, kwa lengo la kuyatumi akama silaha ya maangamizi dhidi ya viogozi wengine, lakini katika kipindi kifupi tu waliweza kuumbuka, baada ya ukweli wa mambo kuwekwa wazi.

Najua na ninatambua kuwa siku zote kama ilivyo katika vilabu vya mpira wa miguu, huwa wapo washabiki damu. Washabiki ambao huwa hawasiki la mwazini wala la mnadi sala. Wako tayari kushabikia jambo fulani hata kama halina ukweli na maslahi kwa nchi. Hawa hatuna jinsi ya kuwabadili msimamo wao na si makusudi ya safu hii kuwabadili watu hao.

Ninachotaka kusema ni kuwa, tumebakiza siku tano tu kufanya maamuzi makubwa na mazito kwa nchi yetu. Naamini kila mmoja wetu kwa njia moja ama nyingine ameshiriki katika kampeni zilizoanza Augosti 20 mwaka huu hata kama si moja kwa moja au kwa kuhudhuria mikutano ya kampeni katika viwanja mbalimbali.

Ni wazi kuwa hapo ulipo sasa tayari umekwisha kufahamu mgombea yupi unapaswa au ungependa kumchagua ili awe kiongozi wako kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Uamuzi ni wako na una kila sababu ya kuwa huru, lakini unapaswa kujiuliza mara mbili, je huyo unayetaka kumchagua ni kwa kiasi gani ataweza kutimiza ahadi alizotoa majukwaani?

Ni vema ukajiuliza katika hili, ili usije ukafanya maamuzia mbayo pengine yataturudisha nyuma kuliko hapa tulipofikia. Ukidhani kwamba mgombea kipenzi chako anaweza kuleta mabadiliko katika Kata yako, Jimbo na hata nchi basi jitokeze kupiga kura ifikapo Oktoba 31, mwaka huu.

Hapa nina maana kwamba, pamoja na uamuzi ulijikita katika kichwa chako hivi sasa, bado unayo fursa ya kutumia hizi siku tano zilizobakia kumpima mgombea udiwani, ubunge na urais ambaye ndiye chaguo lako kama anafaa. Wakati mwingine si lazima kumchagua swahiba wako kuwa kiongozi endapo uanamini au unadhani kuwa hawezi kutimiza ndoto zako.

Tunachopaswa kufahamu ni kuwa, ushabiki wa aina yoyote ile haupaswi kutawala mawazo, fikra na maamuzi yetu katika kuchagua viongozi. Nafikiri tunapaswa kuwa makini zaidi katika kipindi hiki kuliko wakati mwingine wowote, kwakuwa kosa tutakalolifanya litatugharimu kwa miaka mitano ijayo, labda tu itokeo vinginevyo.

Shime mtanzania mwenzangu usiweke nyuma na kushindwa kupiga kura Oktoba 31. Endapo utakuwa mzima wa afya, jitokeze wewe na familia yako na wote waliofikisha umri wa kupiga kura, kutumia haki yenu hiyo ya msingi, kikatiba na kidemokrasi ya kuingiza viongozi madarakani, kwa umakini mkubwa.

Nasisitiza upige kura kwa umakini kwakuwa ukishapiga kura na kwa bahati mbaya ukafanya uchaguzi batili, hautakuwa na fursa ya kufanya mabadiliko kwakuwa mfumo huo wa demokrasia haupo na haujapata kutumika katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Itakulazimu kusubiri kwa miaka mitano ndipo ujisahihishe.

Waungwana, fainali imewadia, uamuzi ni wa kwako. Jitahidi kufanya maamuzi sahihi, ili uendelee kuwa na furaha katika miaka mitano ijayo. Furaha na majuto yako mikononi mwako, huna sababu ya kujuta wakati fimbo unayo mkononi. Kila la kheri katika uchaguzi mkuu, usibaki nyumbani, jitokeze kupiga kura kumchagua yule unayeona anafaa kuwa kiongozi wa eneo lako, jimbo na hata nchi.

Wasalaam,

No comments:

Post a Comment