NINAYO kila sababu ya kumpongeza Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustapha Mkulo kwa hotuba nzuri ya bajeti aliyoitoa bungeni mjini Dodoma wiki iliyopita. Kwa hakika, hotuba hiyo inaonyesha mwanga wa mwelekeo chanya kiuchumi.
Ongezeko la bajeti hiyo kwa kiasi cha shilingi 1.6 trilioni ilinganishwa na bajeti ya mwaka wa fedha 2009/2010, si haba na wala si jambo la kubeza. Ni jambo la kuunga mkono na kutoa ushirikiano wa dhati, kuhakikisha inatekelezwa kama vile inavyopangwa.
Kusimamiwa na kutekelezwa vema kwa bajeti hiyo, hapana shaka pataiwezesha Serikali ya awamu ya nne kufikia malengo yake iliyojiwekea na hasa ya kuleta nafuu ya maisha kwa wananchi wake.
Ni kweli bajeti hiyo imezingatia mambo mengi kiasi cha kuwepo kwa ongezeko katika maeneo muhimu kwa maendeleo ya Taifa na wananchi kwa ujumla. Ukiiangalia kwa makini, utabaini kuwa katika elimu kumekuwepo na ongezeko la aslimia 17.2, miundombinu 37.7%, kilimo 35%, afya 25.2%, nishati 14.6 na maji 14.5. Hili ni ongezeko kubwa katika bajeti na endapo litatekelezwa kama vile ilivyopangwa, tutashuhudia kutokea kwa maajabu Tanzania.
Kwa mtazamo wa haraka haraka, hapana shaka yoyote kwamba bajeti hii inaweza kuleta mabadiliko makubwa katika jamii, pale tu tutakapothubutu kuhakikisha hakuna yeyote anayeweza kucheza nayo au kuzorotesha juhudi za kuitekeleza.
Fikra Pevu inatoa onyo hilo kwa kuzingatia ukweli kwamba katika miaka ya hivi karibuni, wamejitokeza watu wasioitakia mema serikali iliyopo madarakani na kuamua kuihujumu vile wanavyopenda au wanavyoona inafaa. Watu hao ambao wengine ni maofisa waandamizi, wamediriki kuzorotesha mipango na miradi yote ya maendeleo ili mradi serikali ionekane haijafanya chochote.
Kuendelea kuwaacha maofisa wa namna hiyo kuwepo katika ofisi hizo za umma, ni sawa na kuwasaliti wananchi na pia ni kusaliti juhudi zinazofanywa na maofisa wachache waaminifu wa serikali, walioko tayari kutii maagizo ya viongozi na watendaji wakuu wa serikali. Kushindwa kutekelezwa kwa bajeti mathalani hii ya 2010/11, hakutakuwa na dosari kwa maofisa wa serikali, isipokuwa itakuwa doa kwa serikali ya Rais Jakaya Kikwete. Hii yote ni kutokana na yeye kuwa kinara wa serikali hivyo kila baya kubebeshwa yeye hata kama hausiki.
Njia pekee ya kuondokana na hali hiyo, ni kuhakikisha kila ofisa wa serikali pale alipo, anatimiza wajibu wake vile inavyopasa na ndani ya muda wa kazi, yaani saa 2 asubuhi hadi 9:30 alasiri na si kufanya kazi hizo katika muda wa ziada ili kudai exta duty allowances.
Ningekuwa mimi mwamuzi, posho za muda wa ziada zingetolewa tu pale inapoonekana iko haja ya kutolewa kwake hasa kutokana na mtumishi kushindwa kumaliza majukumu yake katika muda wa kawaida, na kwamba aliutumia vema muda huo wa kawaida bila mafanikio. Posho hizo zisingetolewa kwa watumishi wanaotumia muda wa asubuhi kuzungukia miradi yao na kupiga porojo, halafu ikifika saa 9:30 ndiyo wanaanza kuwajibika vile inavyopasa.
Huo ni wizi, tena wizi wa mchana kweupe ambao haufai hata kidogo kufumbiwa macho hasa katika utekelezaji wa bajeti hii ya mwaka 2010/11, ili iweze kuzaa matunda yale yanayotarajiwa.
Inawezekana kabisa viongozi wetu wanayo nia nzuri ya kuleta unafuu wa maisha kwa watanzania. Lakini bado wapo watendaji wachache, wanathamini zaidi nafsi zao, hivyo kuamua kwa makusudi kuvuruga nia nzuri ya viongozi wetu. Kwakuwa baadhi ya watendaji wa namna hiyo wanafahamika, basi hatua kali za kinidhamu zianze kuchukuliwa dhidi yao kuanzia Julai mwaka huu, ili wakumbuke kwamba wapo katika ofisi hizo kuwatumikia watanzania na si kutunisha matumbo yao.
Au pengine uanzishwe utaratibu wa kuwepo kwa masanduku maalum ya maoni, ambapo yatatumika kubainisha majina ya maofisa wanaozorotesha jitihada za serikali ya awamu ya nne katika kutekeleza ahadi zake.
Fikra Pevu itafurahi zaidi endapo mkazo huo utawekwa kwa kuanzia katika Halmashauri zilizopo nchini ili mapato yake yapande kufikia angalau asilimia 20 ya mapato yote ya ndani. Hakika inatia aibu kwa Halmashauri hizo kutarajiwa kukusanya jumla ya shilingi 172.582 bilioni sawa na asilimia 2.9 ya mapato ya ndani yanayokusanywa na Serikali Kuu katika mwaka wa fedha 2010/11.
Kama alivyosema Waziri wa Fedha katika hotuba yake, kiwango hicho ni kidogo ikilinganishwa na fursa zilizopo katika mazingira ya Serikali za Mitaa. Ni vema eneo hilo likatupiwa kurunzi ya aina yake, ili mapato yaweze kuimarika na kuboreka, hivyo kubadili mfumo wa maisha wa wananchi wanaoishi katika Halmashauri hizo.
Pamoja na upungufu unaojionyesha kwenye Halmashauri, bajeti ya 2010/11 iko poa, ni jukumu letu kuitekeleza na kuitafsiri kwa vitendo.
*Mwandishi wa safu hii anapatikana kwa simu: 0713 077588
No comments:
Post a Comment