NIKIWA Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Klabu ya Waandishi wa Habari wa Mkoa wa Dar es Salaam (DCPC), Juma lililopita nilipata fursa ya kuhudhuria mafunzo ya siku moja.
Mafunzo hayo yaliyofanyika mjini Kibaha, Pwani na kudhaminiwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), yalilenga katika kuwafundisha waandishi wa habari wa Dar es Salaam, Pwani, Morogoro na Tanga mwongozo wa maadili katika kuripoti habari za uchaguzi mkuu 2010.
Mwongozo huo muhimu kwa wanahabari na vyombo vya habari hasa katika kipindi hiki cha kampeni kuelekea uchaguzi mkuu, unabainisha maeneo kumi na matano muhimu katika uandishi wa habari makini na unaozingatia kanuni.
Maeneo hayo ni pamoja na kutokupendelea, kuandika ukweli, kuitikia mahitaji ya wapiga kura, kuhamasisha uhuru wa maoni, kulinda vyanzo vya habari, kuepuka matamshi ya chuki na uchochezi, kukuza tunu za demokrasi na wajibu wa vyombo vya habari na wamiliki wake.
Mengine ni kufanya uchunguzi wa hoja, kuwa na bei zinazowiana za matangazo, vyombo vya habari kufanya kazi kulingana na matakwa ya sheria ya uchaguzi, vyombo vya habari kushirikiana na jumuia za kiraia, kuepuka makosa ya kitaaluma, kuwa makini na kura za maoni na vyombo vya habari kukuza ushiriki wa makundi maalum katika kupata nafasi za uongozi wa kisiasa.
Ukiangalia kwa undani vipengele hivyo vya mwongozo wa maadili katika kuripoti habari za uchaguzi mkuu 2010, unabaini kuwa vina umuhimu mkubwa sana si tu kwa vyombo vya habari na wanahabari, bali hata kwa jamii. Lakini swali la kujiuliza UNDP na Baraza la Habari Tanzania (MCT) walikuwa wapi siku zote hadi waje kutoa mafunzo leo hii wakati kampeni zimeanza? Vyombo vitayapigiaje makundi maalum wakati tayari yalishaachwa nje ya ulingo?
Wanaweza kusema kwamba walianza mapema kutoa mafunzo hayo, lakini taarifa zinaonyesha kwamba Jukwaa la Wahariri liliridhia mwongozo huo katika warsha iliyofanyika Agosti 13 mwaka huu mjini Morogoro na kwamba wadau wa habari nao waliridhia katika mkutano uliofanyika jijini Dar es Salaam Agosti 18 mwaka huu.
Kwa yeyote anayetambua umuhimu wa mwongozo wa maadili ya kuripoti habari za uchaguzi mkuu, anaweza kukubalina na Fikra Pevu kwamba mafunzo na kuridhiwa kwa mwongozo huo kumekuja tayari kukiwa kumekucha.
Ni kwa muktadha huo, ni vema basi taasisi zinazohusika zikafikiria namna ya kutoa mafunzo ya jinsi hiyo mapema kabla mchakato wa jambo husika haujanza, ili taasisi hizo ziwe na fursa nzuri ya kufuatilia yupi alifuata maadili na yupi alipotoka.
Huenda haya tunayoyashuhudia hivi sasa ya vyombo vya habari kugawanyika katika mchakato wa kupata viongozi wa taifa hili ni kutokana na maadili hayo kutokufahamika na waandishi pamoja na wahariri wao.
Lakini pengine kunaweza kuwa ndiyo ukomavu wa demokrasia kwa vyombo vya habari kushiriki ipasavyo kumwingiza au kumng’oa madarakani mgombea fulani.
Aina hii ya uandishi wa habari unaonekana hapa nchini hivi sasa, unaweza kuushuhudia nchini Marekani ambapo ni jambo la kawaida wakati wa uchaguzi, gazeti fulani kujiweka wazi kuwa litaendesha kampeni kuhakikisha mgombea fulani anaingia madarakani.
Hiyo huwa haijalishi kama gazeti hilo ni la chama husika ama la. Jambo kubwa linalozingatiwa na gazeti huwa ni sera za mgombea na Ilani ya uchaguzi ya chama, kwamba kikiingia madarakani, kitawafanyia kitu gani wamarekani.
Kwa mantiki hiyo, kama vyombo vya habari vya Tanzania vinadhani demokrasia imepanuka kiasi cha kutosha, ni vema vikaweka wazi upande vinaposhabikia badala ya kuyumbisha wasomaji na wananchi. Ni vema vikasema kuwa tuunga mkono ama Ari Zaidi, Nguvu Zaidi na Kasi Zaidi au Hatudanganyiki, badala ya kudemadema.
Naamini vyombo vya habari vikionyesha kule vipoangukia, itakuwa rahisi kwa UNDP na MCT mwaka 2015 kujua mwongozo wa maadili ya kuripoti habari za uchaguzi uweje, kwa kuwa tayari vyombo vitakuwa vimekwisha kujipambanua.
No comments:
Post a Comment